Sunday 15 December 2013

TATA MADIBA AZIKWA KWA HESHIMA ZOTE BILA KUSAHAU MILA NA DESTURI.



Mandela azikwa kijijini kwao huko Qunu Afrika Kusini.
·    Takribani watu 4,500 wahudhuria mazishi.
·    Azikwa kwa heshima zote, huku mila na desturi za kabila lake zikizingatiwa.

Na. Mwandishi wetu.

Mazishi ya Nelson Mandela yamefanyika leo jumapili katika kijiji cha Qunu katika mkoa wa Eastern Cape na kumaliza wiki moja baada  ya maombolezi ya shujaa wa Afrika marehemu  Nelson Mandela.

Takriban watu 4,500 ikiwemo wageni wa kimataifa wamehudhuria mazishi hayo ambayo ni ya mchanganyiko wa tamaduni za kale na mambo ya kisasa.

Familia ya Mandela ilikesha wakijiandaa kwa mazishi ya leo huku kukiwa na muimbaji ambaye atakuwa anaita mizimu ya mababu wa kale na pia wakiongelesha mwili wa Mandela kumwambia kuwa sasa anazikwa.
 Jeneza la aliyekuwa rais wa kwanza mweusi, Tata Nelson Mandela likisindikizwa na makamanda wa juu wa vikosi vya usalama, wakati wa mazishi yake huko Qunu, Afrika ya kusini.


 Ni kuambatana na tamaduni na mila za watu wa ukoo wa Mandela wa Thembu.

Viongozi wa Afrika, familia na marafiki wametoa heshima zao za mwisho kwa hayati Nelson Mandela katika mazishi yake ya kitaifa katika kijiji cha Qunu katika mkoa wa Cape Mashariki. Mandela alikuwa rais wa kwanza mzalendo wa Afrika Kusini.

Rais Jacob Zuma alisema kuwa wakati safari ndefu ya Mandela kuelekea uhuru imekwisha, raia wa Afrika Kusini wana jukumu la kuendeleza sera zake na urithi wake.

MWENYEKITI WA ZAMANI WA CCM MKOANI MWANZA, CLEMENT MABINA, AUWAWA NA WANANCHI.

Aliyekuwa mwenyekiti wa zamani wa CCM mkoa wa Mwanza  marehemu, Clement Mabina,ambaye ameuwawa kwa kushambuliwa na wananchi wa kanyama Kisesa.


Aliyekuwamwenyekitiwa zamani wa CCM Mkoani Mwanza, auwawa.
·    Ni Clement Mabina.
·    Ashambuliwa na wananchi wenye hasira.
·    Kisa chaelezwa ni ugomvi wa mashamba.


Na. Mwandishi wetu.

MWENYEKITI wa zamani wa chama cha mapinduzi(ccm) mkoa wa Mwanza Clement Mabina ambaye pia ni diwani wa kata ya Kisesa wilayani Magu mkoani Mwanza ameuawa na wananchi wenye hasira katika ugomvi wa mashamba.

Tukio la kuuawa kwa Mwenyekiti huyo wa Ccm Mkoa wa Mwanza ambaye alishindwa katika uchaguzi wa nafasi ya Mwenyekiti wa ccm mkoa wa Mwanza mwaka jana na Waziri wa zamani na Mbunge wa zamani wa Ilemela Dk Antony Diallo lilitokea leo asubuhi katika eneo la kijiji cha Kanyama wilayani Magu.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana na kuthibitishwa na Mkuu wa polisi wa wilaya(OCD) ya Magu ODC Mkapa pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Magu Desdery Kiswaga zimeeleza kuwa tukio limetokea majira ya saa mbili asubuhi.

ODC Mkapa alikiri kutokea kwa tukio la kupigwa na kuuawa kwa Mwenyekiti huyo wa zamani wa Ccm Mkoa na Mwenyekiti wa zamani wa Halmashauri ya wilaya ya Magu baada ya kutokea kutokuelewana baina yake na wananchi wa eneo la kijiji cha Kanyama alikokuwa na shamba lake alikokuwa amekwenda kupanda miti.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Magu Desdery Kiswaga alisema kuwa amepokea taarifa za kuuawa kwa kupigwa na wananchi wenye hasira kutokana na ugomvi wa mashamba na kuelezwa kuwa amesikitishwa sana na kuuawa kwa Mwenyekiti huyo wa zamani wa Halmashauri ya wilaya ya Magu.

Taarifa zaidi toka eneo la tukio la Kanyama kulikotokea mauaji hayo zimeeleza kuwa Mwenyekiti huyo wa zamani wa CCM alifika katika eneo hilo majira ya asubuhi kwa ajili ya kupanda miti katika eneo la milima ya Kanyama ambalo analimiliki ambavyo hata hivyo linadaiwa kuwa na mgogoro baina yake na wananchi.

Baada ya kufika katika eneo hilo,wananchi nao walifika katika eneo hilo na kumhoji sababu za kupanda miti katika eneo hilo ambalo bado lina mgogoro wa umiliki na kutokea kutokuelewana baina yake na wananchi.

Baada ya majibishano ya muda mrefu na kuona wananchi wameanza kumzingira Mabina aliamua kufyatua risasi hewani kuwatawanya wananchi hao ambapo kwa bahati mbaya mojawapo ya risasi hizo zilimpiga mtoto aliyekuwa katika eneo hilo na kupoteza maisha.

Taarifa hizo toka katika eneo hilo la tukio zimeeleza kuwa kutokana na tukio hilo wananchi walimzingira Mabina na kuanza kumpiga kwa silaha mbalimbali za jadi kama vile mapanga, fimbo, mawe, mikuki na kusababisha kifo chake papo hapo.

Kabla ya kurejea chama cha mapinduzi(ccm) na kufanikiwa kuwa diwani wa Kata ya Kisesa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Magu, Mabina aliwahi kuwa mwanachama wa chama cha NCCR-Mageuzi na aligombea nafasi ya Ubunge katika jimbo hilo mwaka 1995 na kushindwa na aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo Malaki Lupondije.