Tuesday 31 December 2013

TASAJA YAJITOSA MGOMO WA WAFANYABIASHARA MWANZA.>>>>

Afisa habari wa TASAJA, Bituro Kazeri aliyenyoosha mikono wakati akizungumza na wandishi wa habari jijini Mwanza.

TASAJA yajitosa mgomo wa wafanyabiashara Mwanza.
·    Yawataka wafanyabiashara warudi kutoa huduma kwa jamii.
·    Yasema hoja waliyonayo wafanyabiashara ni ya msingi, lakini njia waliyoitumia sio sahihi.

Na. Baltazar Mashaka.

TAASISI  Sayansi ya Jamii (TASAJA) ya Jijini Mwanza, imeingilia kati mgomo wa wafanyabiashara ikitaka watafakari na kusitisha mgomo huo, kwa madai kuwa hauna tija kwa maslahi ya nchi na jamii.

TASAJA pia   imewataka warudi kutoa huduma kwa jamii na serikali ibebe mzigo wa kusambaza mashine hizo kielektroniki ,Electronic  Fiscal Device (EFD) kwani haitapoteza chcochote, ili kuondokana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mgomo huo.

Afisa habari wa TASAJA, Bituro Kazeri, akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Mwanza,  alisema hoja ya wafanyabiashara hao  kuhusu gharama kubwa za kununulia mashine za Ankara za kutolea kodi ni ya msingi, lakini njia waliyotumia ya mgomo, si njia sahihi ya kutatua  matatizo bali ni kufungua mlango mwingine wa  matatizo.

“Wafanyabiashara kwa muda mrefu sasa wamekuwa wakinung’unika  kupinga matumizi ya  mashine  maalum za Ankara za  kutolea kodi (EFD ) wanapouza bidhaa zao. Ununuzi wa  mashine hizo umezua  migomo na kuathiri huduma za kijamii na kiuchumi na kwa siku hizo ya serikali haikuingiza mapato.

Mgomo huo utakuwa na madhara makubwa kwa jamii siku za karibuni,kama mishahara, ukosefu madawa  hospitali na huduma zingine za msingi ”alisema Kazeri.

Alisema serikali pekee ikiachiwa mzigo huo wa kuagiza mashine hizo lazima gharama kubwa zitarudi kwa walaji na ni kuwabebesha mzigo mkubwa  wa kodi. Lakini pia watumiaji wakiachiwa wazinunue kinachogomba ni upatikanaji wake. 

“Sidhani  kama tutafikia hatua mashine  hazitatumika, na matokeo tunayotaka kwa njia ya mgomo hayataondoa hilo. Ndiyo maana TASAJA tunaitaka serikali irudi kule inakokopa ,ikiwezekana izungumze na benki ya dunia watukopeshe tununue mashine hizo tutalipa,”alisema Kazeri.

Aidha alisema wao TASAJA wanaunga mkono hoja za Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato (TRA) kuwa matumizi ya mashine hizo yanalenga kupunguza mianya ukwepaji kodi na mianya ya rushwa miongoni mwa wakusanya kodi wasio waaminifu, kuongeza na kuboeresha ukusanyaji kodi na utunzaji kumbukumbu za mauzo na manunuzi .

Kazeri alidai kuwa teknolojia hiyo ya kutumia mashine za kutolea Ankara za kodi ikitumika vizuri, itaboresha ukusanyaji  kodi  na kuweka kumbukumbu sahihi zinazotiliwa shaka na maofisa wa kodi . Kwamba njia hiyo ndiyo inayotumika duniani kote na itaondoa manung’uniko na lawama kati ya wafanyabiashara na watoza kodi.

“Mfumo huu ukiangaliwa kisayansi litakuwa ni jambo bora,Tunachokata ni upatikanaji wake.Ukinunua serikali itakulipa kupitia kodi unayopaswa kuilipa.Hii ni faida kwa serikali,wafanyabiashara na lazima watumiaji wafahamu faida zake na elimu ya matumizi ya mashine hizo za Ankara za kutolea kodi,”alifafanua Kazeri.

Alisema kuwa miradi mingi ya kuboresha ukusanyaji wa mapato nchini imekuwa ikipatya ufadhili wa Benki ya Dunia, hivyo ni vema Serikali ikaangalia uwezekano wa kufanya nayo mazungumzo au wahisani wengine ipate fedha za kununulia mashine hizo ni kuzigawa bila kujali ukubwa wa biashara.

Alisema matumizi ya mashine hizo kwa kiwango kikubwa yataiwezesha nchi kuongeza ukusanyaji kodi,kujenga na kukuza utamaduni wa kuchukua Ankara za mauzo na manunuzi ,ambao kwa hapa nchini ni wa kiwango cha chini na utajenga uhusiano mzuri baina ya wadau wa kodi ambao ni serikali,wafanyabiashara,watoza kodi na jamii.

“Kodi ndiyo uhai wa serikali na ustawi wa wananchi wake.Hakuna njia nyingine ya serikali kupata kodi mbalimbali bila kuwatoza wananchi wake kwa njia sahihi na uwazi mkubwa.TASAJA tunapendekeza matumizi ya mashine za kutolea Ankara ni njia muafaka ya kuleta ukusanyaji  kodi sahihi na wa haki .Kila mdau anapaswa kuliunga mkono zoezi hili,”alisema Kazeri.

Wafanyabiashara wamekuwa wakituhumiwa kutumia vitabu viwili vya Ankara za kodi ,kutiliwa shaka kwa kumbukumbu zao  za biashara na maofisa wa kodi  hali ambayo imekuwa ikisababisha wakadiriwe kodi siyosahihi.

Kwamba TRA nao wanatuhumiwa kuwapandishia kodi wafanyabiashara katika makadirio ya kodi. Makadirio hayo makubwa yalikuwa yakijenga mazingira na njia ya kushawishi na kulazimisha rushwa,mambo yanayopingwa na wafanyabiashara.

Hata hivyo Kazeri alisema ujio wa mashine za kutolea Ankara za kodi ndiyo jibu muafaka la matatizo yanayouzingira mfumo wa ukusanyaji kodi na uhusiano kati ya wafanyabiashara na watoza kodi na ni njia ya kisayansi ya kushughulikia suala hilo.

Monday 30 December 2013

ERNEST MANGU NDIYE KAMANDA MPYA WA JESHI LA POLISI NCHINI TANZANIA.>>>>>>>

Ernest Mangu, Mkuu mpya wa jeshi la polisi nchini Tanzania. ( Picha na maktaba yetu)


Rais Kikwete amteua Kamishina wa Polisi Ernest Mangu kuwa mkuu mpya wa jeshi hilo.
·    Kuapishwa jumanne hii  viwanja vya Ikulu Dar.
·    Nafasi ya naibu mkuu wa jeshi la polisi yaanzishwa.

Na. Ofisi ya Ikulu.

Rais wa jamuhuri ya muungano wa Tanzanzania Jakaya Mrisho Kikwete leo jumatatu Desemba 30, 2013,  amemteua Kamishina wa Polisi Ernest Mangu kuwa Mkuu wa jeshi la Polisi nchini Tanzania, IGP.

Kulingana na taarifa iliyotolewa na katibu mkuu kiongozi Balozi Ombeni Sefue inaeleza kuwa Kamishina Mangu anachukua nafasi ya mkuu wa Jeshi la Polisi nchini anayestaafu, Said Mwema.

Kabla ya uteuzi wake unaoaanza januari mosi 2014, Kamisha Mangu alikuwa Mkurugenzi wa Intelijensia ya jinai (Director of Criminal Intelligence) katika jeshi hilo la polisi.

Aidha taarifa hiyo inasema kuwa Rais Kikwete amemteua Kamishina Abdulrahman Kaniki kuwa Naibu Mkuu wa wa Jeshi la Polisi nchini Tanzania ikiwa ni nafasi mpya katika muundo wa sasa wa jeshi hilo.

Kabla ya uteuzi wake, Kamishina Kaniki alikuwa Kamishina wa Uchunguzi wa Kijinai (Commissioner  for  forensic Investgations.)

Mkuu wa Jeshi la Polisi mpya ataapishwa jumanne hii Desemba 31, 2013 katika viwanja vya Ikulu jijini Dar es salaam.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano,
Ikulu.
Dar es Salaam.

WAFANYABIASHARA MWANZA WAITIKISA SERIKALI.>>>>>>>>>

Bw. Filip Chibululu almaarufu Mandela, akiwa ameshika bango, kama linavyojieleza hapo, kama alivyonaswa na kamera ya Kisima cha habari katika maeneo ya Mwanza hotel jana, wakati wafanyabiashara walipoanza mgomo wao.


Wafanyabiashara Mwanza waitikisa serikali.
·    Wagoma kufungua maduka kisa mashine mpya za kielektronik zinazohusiana na masuala ya kodi.
·    Walia na bei za mashine hizo.

Na. Baltazar Mashaka.

WAFANYABIASHARA na Matajiri wa Jijini la Mwanza, wameitikisa Serikali, wakipinga ununuzi wa mashine za Kielektroniki, Electronic Fiscal Device (EFD) na manyanyaso kutoka taasisi za umma .

Wafanyabiashara hao jana asubuhi, walianza mgomo na kutofungua maduka yao hadi hapo serikali itakapokutana na kukaa meza moja, ili kutafuta suluhu ya unyanyasaji wanaofanyiwa na Mamlaka ya Mapato (TRA), Halmashauri ya Jiji na Jeshi la Polisi mkoani hapa.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Kisima hiki cha habari jijini Mwanza jana, wafanyabiashara hao walisema mgomo huo usio na kikomo utafikia mwisho baada ya serikali kuona umuhimu wa kukutana nao.

Walidai kuwa maofisa wa TRA wana wanyanyasa kwa kuwakadiria kodi kubwa kuliko wanapoingiza shehena ya bidhaa kutoka nje ya nchi, na wakati mwingine hutakiwa kupeleka nyaraka za mizigo hiyo Dar es salaam.

Pia wanadai kulazimishwa kununua mashine za EFD kwa bei kati ya sh. 800,000 hadi 1,000,000 ,wakati mashine hizo bei yake halisi haizidi sh.200,000 na kuhoji TRA wana maslahi gani na mashine hizo.

Malalamiko mengine ni dhidi ya  halmashauri ya jiji  kuwatoza ushuru wa mizigo wanayotoa stoo na kuingia dukani,huku polisi nao wakidaiwa kuwaomba stakabadhi kwa bidhaa zinazoingizwa dukani kutoka stoo.

“TRA,Jiji na Polisi wametugeuza shamba la bibi. Unapo crea mzigo mpakani bila kuwapa cha juu unakadiriwa kodi kubwa. Ukifika hapa wanadai aliyekagua mzigo amekosea ili mradi uwape hela. Halmshauri nao wanataka ushuru hata kwa bidhaa unazoingiza dukani, ni unyanyasaji tu.” Alisema mmoja wa wafanyabiashara hao.

Walidai Mkuu wa Mkoa wa Mwanza (RC), Mhandisi Evarist Ndikilo, pamoja na kuandikiwa barua na wafanyabiashara hao kupitia kwa Mwanasheria wao,wakimtaka akutane nao Desemba 20, mwaka huu,hakuwajibu badala yake akaenda kufanya siasa na waendesha pikipiki.

Kampuni ya Uwakili ya Kabonde na Magoiga, ilikiri kumwandikia barua Mkuu wa mkoa  ikimtaka akutane na wateja wao ili kujadili na kutafuta ufumbuzi malalamiko yao.

“Wateja wetu walitupa maelekezo yao na sisi tukamwandikia barua RC tukimtaka akutane nao Desemba 2013 mwaka huu, lakini alitujibu kwa barua yenye kumb BE 222/226/01/26 ya tarehe 27 Desemba. Tumeipokea saa 3:00 asubuhi wakati  tayari wateja wetu wakiwa wameanza mgomo,”alisema mmoja wa mawakili wa kampuni hiyo kwa sharti la kutotajwa jina kwa vile si msemaji.

Alisema RC alipaswa kujibu barua hiyo kabla ya mgomo na kunusuru usumbufu na kero wanayopata wananchi, sababu  mgomo  huo  una athari kubwa kiuchumi kwa taifa na kijamii na pengine hakuona umuhimu wa wafanyabiashara hao kuhudumia  wananchi.

“Mkuu wa mkoa alifanya siasa badala ya kuangalia uchumi wa nchi na athari zake kutokana na mgomo wa wafanyabiashara hao. Hakuona umuhimu wake. Leo wananchi wanahangaika ukizingatia shule zinafunguliwa na wanafunzi wanamahitaji ya shule na mahitaji mengine muhimu ya  jamii.”Alisema.

Habari za uhakika kutoka ofisi ya RC zinasema, alikuwa akikutana na viongozi wa wafanyabiashara hao mchana huu kwenye ukumbi wa ofisi yake, kujadiili kadhia hiyo pampoja na malalamiko yao.

Kisima cha habari kilishuhudia baadhi ya wafanyabiashara wakiwa wamekusanyika kwenye kituo cha zamani cha mabasi cha Tanganyika, huku mitaa yote ya katikati ya jijiji maduka yakiwa yamefungwa, ukiondoa wafanyabiashara ndogo ndogo (Machinga ) ambao waliendelea kufanya biashara katika mtaa wa makoroboi na maeneo mengine.

Lakini si maeneo ya mjini kati tu, aidha eneo la Nyakato National pia lilionekana idadi kubwa ya maduka ikiwa imefungwa katika kile kilichoelezwa ni kuunga mkono mgomo huo  wa wafanya biashara.

Sunday 29 December 2013

RAGE BADO NI MWENYEKITI HALALI WA SIMBA.>>>>>>>>>

Mwenyekiti halali wa Klabu ya Wekundu wa Msimbazi, Simba, Ismail Aden Rage.


Rage ndiye mwenyekiti halali wa Simba.
·    Maamuzi yaliyochukuliwa na kamatia ya utendaji ya Simba kumsimamisha yaelezwa ni batili.
·    Agizo la TFF kumtaka Rage aitishe mkutano mkuu wa wanachama bado lipo palepale.
·    Nalo sakata la Okwi, TFF ladai kulitambua.

Na. Deo Kaji Makomba.

Ismail Aden Rage ndiye Mwenyekiti halali wa Simba ambapo Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji imemtaka kuitisha Mkutano Mkuu kwa mujibu wa taratibu za klabu ya Simba.

Kauli hiyo ya Kamati ya sheria na hadhi za wachezaji inakuja kufuatia kubaini  mapungufu kadhaa ya kisheria kwenye uamuzi wa Kamati ya Utendaji ya Simba uliofanywa Novemba 18, 2013 kwa kumsimamisha Mwenyekiti wao, katika kikao cha kamati hiyo kilichofanyika jumamosi iliyopita jijini Dar es salaam.

Kulingana na taarifa iliyotolewa na Shirikisho la soka nchini Tanzania, TFF, na kusambazwa na ofisa habari wa Shirikisho hilo, Boniface Mgoyo Wambura na kasha nakala yake kukifikia Kisima cha habari, imebainisha  Upungufu huo kuwa  ni pamoja na ukiukwaji wa Ibara ya 33 ya Katiba ya Simba juu uitishaji wa mkutano, ajenda ya kumsimamisha Mwenyekiti kuwasilishwa kwenye kikao kwa utaratibu wa mengineyo.

Changamoto nyingi zilizoelekezwa kwa Mwenyekiti huyo zingeweza kupatiwa ufumbuzi kwa kutumia Ibara ya 16(2) ya Katiba ya Simba.

Hivyo, agizo za Rais wa TFF, Jamal Malinzi kumtaka Mwenyekiti wa Simba aitishe mkutano lipo palepale.

Pia Mwenyekiti ametakiwa kufanya uchaguzi wa kujaza nafasi ya Makamu Mwenyekiti kwa kuzingatia Katiba ya klabu hiyo.

Katika mkutano huo wa kujaza nafasi, ndiyo utakaojadili mgogoro kati ya Mwenyekiti na Kamati yake ya Utendaji. Nafasi hiyo kwa sasa inakaimiwa na mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo, Joseph Itang’are baada ya Geofrey Nyange aliyekuwa akiishikilia kujiuzulu.

TFF inakumbusha wanachama wake wote (vyama vya mikoa, vyama shiriki na klabu za Ligi Kuu) kuzingatia Katiba zao. Kamati pia imegundua ukikwaji wa maadili katika suala hili, hivyo, litapelekwa katika kamati husika.

Kwa vile maslahi ya TFF ni kuona mpira wa miguu unachezwa kwa utulivu, itazikutanisha pande husika wakati wowote kuanzia sasa.

Ama kuhusu mchezaji Emmanuel Okwi ambaye aliuzwa nchini Tunisia, TFF inafahamu kuwa klabu ya Simba bado haijalipwa na itasaidia kufuatilia FIFA fedha za mauzo ya mchezaji huyo.

Wakati huo huo, Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF imekitaka Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) kuwasilisha ajenda na muhtasari wa vikao vilivyofanya uamuzi wa kumvua madaraka Katibu wake Riziki Majalla.

Ajenda na muhtasari unaotakiwa ni wa vikao vya Kamati ya Utendaji iliyomsimamisha Katibu huyo kutokana na tuhuma mbalimbali dhidi yake, na Mkutano Mkuu ambao ulimvua madaraka.

Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imekutana Jumamosi (Desemba 28, 2013) kujadili mambo mbalimbali yaliyofikishwa mbele yake ikiwemo usajili wa dirisha dogo ambapo klabu zenye matatizo zimepewa hadi Januari 10 mwakani kurekebisha.

Baadhi ya klabu ikiwemo Simba zimezidisha idadi ya wachezaji, hivyo zimepewa hadi muda huo kupunguza ambapo zikishindwa kazi hiyo itafanywa na Kamati yenyewe.

Simba ina nafasi tano za kujaza kwenye dirisha dogo lakini imewasilisha majina ya wachezaji sita.

Pia klabu nyingine zimetakiwa ama kuvunja mikataba ya wachezaji au kuendelea kuwa nao, na si kuendelea kuwalipa mishahara wakati imeshawaondoa katika orodha yao.