Thursday 31 October 2013

FUJO ZATOKEA UWANJA WA TAIFA. POLISI WATUMIA MABOMU YA MACHOZI




Polisi wa kutuliza ghasia wakifyatua mabomu ya machozi kutuliza fujo uwanja wa taifa hapo jana, wakati Simba ikicheza na Kagera suger katika mechi ya Ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara

Bao la kusawazisha la Kagera Suger katika dakika za lala salama lawachefua mashabiki wa Simba.
·    Baadhi yao wajawa na jazba na kung’oa  viti na kuanza kuvirusha hovyo.
·    Polisi wa kutuliza ghasia watumia mabomu ya machozi kutuliza fujo .
·    Wadau wa soka waeleza hisia zao kutokana na tukio hilo.
·         Wasema si kitendo cha uanamichezo.
                                
                                                   Na. Mwandishi wetu.

Kitendo cha mashabiki wa  timu ya soka ya Simba ya jijini Dar e salaam kufanya fujo na  kung’oa baadhi ya  viti vya uwanja wa Taifa na kuanza kuvirusha  hovyo kimepokelewa kwa hisia tofauti na wapenzi na mashabiki wa soka nchini Tanzania huku wakieleza kuwa kitendo hicho kilichofanywa na mashabiki hao ni utovu wa nidhamu na wanapaswa kuchukuliwa hatua.

 Wakizungumza kwa nyakati tofauti na kisima hiki cha habari alhamis hii mara baada ya kumalizika kwa mchezo kati ya timu ya Simba na Kagewra suger wa ligi kuu soka ya Vodacom Tanzania bara, wapenzi na mashabiki hao  wa soka wamesema kuwa si kitendo cha kiungwana watu wakiangalia burudani halafu kikundi Fulani cha watu kuanzisha fujo na hivyo kuharibu burudani.
 Mmoja wa mashabiki wa timu ya Simba aliyeonekana akifanya fujo hapo akidhibitiwa na polisi wa kutuliza ghasia.

Baadhi ya mashabiki wa timu ya Simba alhamisi hii walijikuta wakishindwa kutuliza jazba zao, baada kuanza kunyofoa viti ndani ya uwanja wa taifa na kuanza kuvirusha hovyo, kufuatia   timu ya Kagera suger kusawazisha bao, lililopatikana kwa njia ya penait kunako dakika za lala salama hali iliyowajaza jazba wapenzi na mashabiki hao wa Simba kuanzisha vurugu kwa mtizamo wa   kuwa, penait iliyotolewa haikuwa sahihi.

Miongoni mwa wadau wa soka aliyezungumza na Kisima cha habari jijini Mwanza,  ni Isack Victor, ambaye amesema kuwa kitendo walichokifanya mashabiki hao si cha kiungwana.

 Baadhi ya viti vya uwanja wa taifa vilivyong'olewa na mashabiki wanaodaiwa kuwa ni wa timu ya Simba.

Victor ambaye pia ni mchambuzi wa soka jijini Mwanza, amesema alivyouona mchezo kupitia Luninga inavyoonekana mashabiki hao hawakuridhishwa na maamuzi yaliyotolewa  na mwamuzi wa mpambano huo ya kutoa penaiti dakika za lala salama hali iliyowafanya mashabiki hao wahamaki na kujawa hasira na kufanya yaliyotokea.

“ Walitakiwa watulize jazba zao, kwani kitendo walichokifanya wala hakiwezi kubadilisha matokeo.” Alisema Isack na kuongeza kuwa “kitendo hicho si cha kiungwana na kiuanamichezo na kinaweza kuwagharimu watu waliofanya fujo hizo kwa kuchukuliwa hatua za kisheria.

  Mshambuliaji wa timu ya Kagera suger akijaribu kumtoka mlinzi wa timu ya Simba, ambapo timu hizo zilitoka sare ya 1 - 1, kwenye uwanja wa taifa hapo jana.

Katika mchezo huo ambao Simba wakitoka sare ya goli 1 – 1 na Kagera Suger, polisi wa kutuliza ghasia walilazimika kutumia mabomu ya machozi ili kuwatuliza mashabiki hao waliamua kung’oa viti na kuanza kuvirusha hovyo hali iliyozua tahaluki ndani ya uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Tuesday 29 October 2013

IMANI ZA KISHIRIKINA ZAENDELEZA UNYAMA KWA BINAADAM.





 Wanaoonekana katika picha watu wawili ambao majina yao yamehifadhiwa, wakiwa na mkono wa binadamu(Picha na mpiga picha wetu.)
Biashara ya viuongo vya binadamu bado yaendelea mikoa ya kanda ya ziwa.

  • Polisi mkoani Mwanza wafanikiwa kukamata watu watatu wakiwa na kiungo cha binaadamu.

  •  Kilikuwa kikiuzwa kwa gharama ya shilingi milioni 100.

                        
                                       Na. Mashaka Baltazar.

JESHI la Polisi Mkoa wa Mwanza,linawashikilia waganga wa jadi wawili na mkulima mmoja, baada ya kuwakamata wakiwa na kiungo cha binadamu,wakitaka kukiuza kwa shilingi milioni 100.

Watuhumiwa hao walikamatwa juzi Oktoba 28 mwaka huu, majira ya saa 9 alasiri eeneo la ziwani jirani na uwanja wa Ndege wa Mwanza katika Manispaa ya Ilemela.

Akizungumza na waandishi wa habari jana,Ofisa Upelelezi Makosa ya Jinai (RCO) na Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza, Kamishna Msadizi wa Polisi, Joseph Konyo,alisema watuhumiwa hao walikamatwa baada ya kupata taarifa na kuwafuatilia.

Alisema Oktoba 20 mwaka huu,walipata taarifa kuwa mtu mmoja alikuwa akijihusisha na biashara ya viungo vya binadamu katka eneo la Igombe Manispaa ya Ilemela.

Kwamba baada ya taarifa hizo, jeshi la polisi lilimtuma mtu wake kwa ajili ya kufanya manunuzi ya viungo hivyo, kutoka kwa mganga mmoja (jina linahifadhiwa)

“Hivi karibuni tulifanya vikao na waganga wa jadi kuzungumzia umuhimu wa kushirikiana na kupeana taarifa za kubaini waganga wanaopiga lamli chonganishi na wakata mapanga, Lengo likiwa ni kukomesha mauaji ya vikongwe,”alisema ACP Konyo na kuongeza;

“Oktoba 20, mwaka huu baada ya vikao tulipokea taarifa kuwa mganga wa jadi huko Igombe anauza viungo vya binadamu. Tulimtuma mtu wetu akiomba kununua,ambapo mganga huyo aliweka muda maalum wa kuleta kichwa cha binadamu,mkono na nyeti.”

Alieleza kuwa kikosi cha jeshi hilo kikiwa kazini mganga huyo aliwaarifu kuwa amekamilisha kazi hiyo, hivyo wakutane kwa ajili ya kufanya biashara na kudai kuwa angeambatana na watu wengine wawili na akapanga mahali pa kukutania.

“Alituarifu kuwa anavyo viungo hivyo tukamfuata mahali tulipokubaliana . Tuliwakuta wote watatu  wakiwa na begi ambapo,mganga huyo alitaka apewe shilingi milioni 100 mtu wetu akaomba apunguze bei ndipo tukawaweka chini ya ulinzi,”alisema

Alisma walipowapekuwa ndani ya begi hilo walikuta kukiwa na chungu na ndani ya chungu kulikuwa na mfuko wa plastiki na ndani ya mfuko huo kulikuwa na mwingine mweupe wa nailoni ndani yakee wakakuta kiganhja cha mkono wa kuume wa bnidamu.

“Tuliwaweka chini ya ulinzi na tukafuata taratibu za upekuzi. Katika upekuzi ndani ya begi lao tulikuta chungu ambacho ndani yake kulkuwa na mfuko mweusi,ndani ya mfuko huo kulikuwa na mfuko wa nylon, mweupe ambao tuliukuta ukiwa na kiganja cha mkono wa kulia wa binadamu kikiwa hakijaharibika na walituonyesha ni  binadamu gani,”alisema ACP Konyo

Hata hivyo alikataa kutaja majina ya watuhumiwa hao kwa madai ya kuvuruga upelelezi, kwa kuwa bado wanamtafuta mfanyabiashara mmoja wa jijini hapa,baada ya kutajwa na watuhumiwa kuwa anajihusisha na biashara hiyo ya viungo vya binadamu.

Miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na mauaji ya kinyama kwa watu wenye ulemavu wa ngozi albino nchini Tanzania, huku ikielezwa kuwa mauji hayo yamekuwa yakifanywa kutokana na imani potofu za kishirikina kuwa kiuongo cha binadamu mwenye ulemavu wa ngozi ya albino kinaweza kuwapatia utajiri.

Hadi hivi sasa serikali ya Tanzania pamoja na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali yamekuwa yakipambana na mauaji hayo ya kinyama ikiwa ni pamoja na kuwakamata watuhumiwa wa mauaji hayo pamoja na kuwafikisha mahakamani na hukumu kutolewa.

Monday 28 October 2013

HATIMAYE RAIS MPYA WA TFF APATIKANA



Rais mpya wa shirikisho la soka nchini Tanzania, TFF, Jamali Malinzi.
Malinzi ndiye rais mpya wa TFF.

  •      Atoa msamaha kwa waliokuwa wamefungiwa katika masuala ya soka.

  • Nafasi ya ujumbe kwa kanda ya ziwa, Nyalla nje, Lufano ndani.


                     Na. Mwandishi wetu.

Jamal Emil Malinzi ndiye Rais mpya wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Malinzi ameshinda wadhifa huo katika uchaguzi wa Kamati ya Utendaji ya TFF uliofanyika juzi (Oktoba 27 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Aliibuka na ushindi wa kura 73 dhidi ya mpinzani wake pekee Athuman Jumanne Nyamlani aliyepata kura 52. Nafasi ya Makamu wa Rais imetwaliwa na Wallace Peter Karia aliyepata kura 67 na kuwashinda Ramadhan Omari Nassib kura 52 huku Imani Omari Madega akipata kura sita.

Akizungumza mara baada ya kuchaguliwa, Rais Malinzi ametaka ushirikiano kutoka kwa wadau wote akiwemo mpinzani wake Nyamlani katika kuhakikisha mpira wa miguu nchini unasonga mbele.


 Rais wa TFF aliyemaliza muda wake Leodiga Chila Tenga, akimkabidhi mpira rais mpya wa TFF, Jamal Malinzi mpira baada ya kufanyika uchaguzi mkuu wa TFF jumapili iliyopita
Rais mpya wa TFF, Jamali Malinzi akiwa na kamati kuu mpya tendaji ya shirikisho hilo.

Pia ametoa msamaha kwa watu wote waliokuwa wamefungiwa kuanzia ngazi ya wilaya, mkoa na TFF. Msamaha huo hauwahusu wale waliofungiwa kwa makosa ya rushwa au kupanga matokeo. Vilevile msamaha huo hauhusu adhabu zilizotolewa katika ngazi ya klabu.

Rais Malinzi pia amevunja kamati zote za TFF ambapo ataziunda upya kwa kushirikiana na Kamati ya Utendaji.

Kwa upande wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji walioshinda ni Kalilo Samson (Kanda namba 1- Geita na Kagera) aliyepata kura 102 za ndiyo na 17 za hapana. Kanda namba 2- Mara na Mwanza, mshindi ni Vedastus Lufano aliyepata kura 51 dhidi ya Jumbe Odessa Magati (11), Mugisha Galibona (24), na Samwel Nyalla (39).

Epaphra Swai ndiye mshindi wa Kanda namba 3- Shinyanga na Simiyu kwa kura 63 dhidi ya Mbasha Matutu aliyepata 61. Kanda namba 4- Arusha na Manyara mshindi ni  Omali Walii Ali aliyepata kura 53 dhidi Elley Mbise (51), Ally Mtumwa (19).

Kanda namba 4- Kigoma na Tabora, mshindi ni Ahmed Idd Mgoyi aliyepata kura 92 dhidi ya 28 za Hamisi Yusuf Kitumbo.

Ayubu Nyaulingo na Blassy Mghube Kiondo ameshinda Kanda namba 6- Katavi na Rukwa kwa kura 73 dhidi ya Ayubu Nyaulingo aliyepata 52. Ayoub Shaibu Nyenzi ndiye mshindi wa Kanda namba 7- Iringa na Mbeya kwa kupata kura 59 na kuwapiku David Samson Lugenge (8), John Exavery Kiteve (12) na Lusekelo Elias Mwanjala (46).

Kanda namba 8- Njombe na Ruvuma inawakilishwa na James Patrick Mhagama aliyepata kura 93 dhidi ya 31 za Kapteni mstaafu Stanley William Lugenge. Athuman Kingombe Kambi ndiye mshindi wa Kanda namba 9- Lindi na Mtwara kwa kura 84 akiwazidi Francis Kumba Ndulane (30) na Zafarani Mzee Damoder (11).

Hussein Zuberi Mwamba ametetea ujumbe wa Kanda namba 10- Dodoma na Singida kwa kura 63 akiwapiku Stewart Masima (58) na Charles Komba (4). Geofrey Irick Nyange ameshinda Kanda namba 11- Morogoro na Pwani akipata kura 78 dhidi ya Juma Pinto (26), Farid Nahdi (14), Riziki Juma Majala (5) na Twahil Twaha Njoki (2).

Kanda namba 12- Kilimanjaro na Pwani, Khalid Abdallah Mohamed ndiye aliyeibuka kidedea kwa kura 69 dhidi ya 54 za mpinzani wake Davis Elisa Mosha.  Kidao Wilfred Mzigama ameshinda Kanda namba 13- Dar es Salaam kwa kupata kura 60 dhidi ya wapinzani wake Muhsin Said Balhabou (50), Omar Isack Abdulkadir (10) na Alex Crispine Kamuzelya (4).